Thursday, April 22, 2010

Inter Milan Yaipasua Kichwa Barcelona

Vijana wa Jose Mourinho, Inter Milan wamewashindilia mabao 3-1 mabingwa watetezi Barcelona katika mechi ya kwanza ya nusu fainali ya kombe la mabingwa ulaya iliyochezwa usiku huu.
Mabingwa watetezi Barcelona ya Hispania ambayo iliigaragaza timu ya Arsenal ya Uingereza kwa jumla ya mabao 6-3 na kuitupa nje ya mashindano ya mabingwa wa ulaya, imeshindwa kutamba nchini Italia na kukubali kipigo cha mabao 3-1.

Barcelona ndiyo iliyokuwa ya kwanza kuliona lango la Inter Milan dakika 18 tu baada ya kipyenga cha kuanza kwa mechi mfungaji akiwa ni Pedro.

Goli hilo liliwafanya vijana wa Mourinho waje juu na kujipatia goli la kusawazisha kupitia kwa Wesley Sneijder kwenye dakika ya 29.

Hadi wakati kipyenga cha mapumziko kinapulizwa, Barcelona na Inter walikuwa sare ya mabao 1-1.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi zaidi na walikuwa ni Inter Milan waliofanikiwa kujipatia magoli mawili ya haraka haraka kupitia kwa Maicon and Diego Milito.

Macho yote leo yalikuwa kwa mchawi wa chenga mwenye umbile dogo, Lionel Messi ambaye alifunga magoli manne peke yake katika mechi ya robo fainali dhidi ya Arsenal.

Lakini mabeki wa Inter Milan walifanikiwa kumbana Messi asifanye makeke yake yaliyompatia jina duniani.

Jose Mourinho hivi sasa ana kazi ngumu zaidi ya kuhakikisha anaiongoza vyema Inter Milan kulinda ushindi wake kwenye mechi ya marudiano itakayofanyika wiki ijayo kwenye uwanja wa Nou Camp nchini Hispania

source nifahamishe

Monday, April 19, 2010

Skendo la Ngono Laikumba Timu ya Taifa ya Ufaransa


Skendo kubwa la ngono limeikumba timu ya taifa ya soka ya Ufaransa ambapo baadhi ya nyota wa timu hiyo ya taifa wanadaiwa kufanya mapenzi na machangudoa wenye umri mdogo.
Baadhi ya wachezaji wa timu ya taifa ya soka ya Ufaransa wamehusishwa kwenye skendo la kufanya mapenzi na makahaba wenye umri chini ya miaka 18.

Mchezaji nyota wa Ufaransa, Franck Riberry na Sidney Govou ni wachezaji wawili waliotajwa ambao tayari wameishahojiwa na polisi kuhusiana na skendo hilo.

Riberry anayeichezea Bayern Munich ya Ujerumani ana mke lakini naye amenaswa katika skendo hilo akidaiwa kufanya mapenzi na msichana kahaba mwenye umri chini ya miaka 18.

Taarifa zilisema kuwa wachezaji wa timu ya taifa ya Ufaransa "Les Bleus" walikuwa wakienda sana kwenye klabu moja ya starehe ya jijini Paris ambapo walikuwa wakiandaliwa makahaba wenye umri chini ya miaka 18. Mmoja wa makahaba hao inadaiwa alikuwa na umri wa miaka 14.

Wachezaji wengine nyota wa Ufaransa nao wamehusishwa na skendo hilo lakini majina yao yamewekwa kapuni.

Mmoja wa wachezaji hao alikiri kufanya mapenzi na msichana mwenye umri mdogo lakini alijitetea kuwa wakati huo alikuwa akiamini kuwa mwanamke aliyeletewa ni mtu mzima.

Kuwadi "Pimp" anayedaiwa kuwaandalia wachezaji machangudoa hao ametiwa mbaroni na baadhi ya wasichana hao wanaendelea kuhojiwa na polisi.

Skendo hilo limekuja ikiwa ni miezi miwili tu kabla ya Ufaransa kuja barani Afrika kwaajili ya fainali za kombe la dunia.


source nifahamishe

Sunday, April 18, 2010

Tottenham Yaharibu Sherehe za Chelsea

Tottenham Hostspur ya jijini London imevuruga mahesabu ya wazee wa darajani Chelsea kutwaa ubingwa wa ligi ya Uingereza kwa kuizamisha kwa mabao 2-1 huku Manchester United ikiwazamisha watani wake wa jadi Manchester City kwa bao 1-0.
Vinara wa ligi ya Uingereza Chelsea leo wamepigwa mwereka na Tottenham Hotspur na kuzamishwa mabao 2-1 na hivyo kuyafanya matumaini ya Chelsea kutwaa ubingwa wa Uingereza mapema kuyeyuka.

Kabla ya mechi Chelsea ilikuwa ikiongoza ligi ya Uingereza kwa tofautiya pointi nne na Manchester United lakini kipigo cha Chelsea na kushinda kwa Manchester United dhidi ya watani wao wa jadi Manchester City kumelifanya pengo la pointi kati ya Chelsea na Manchester United kupungua hadi pointi moja.

Chelsea imebakiza mechi tatu dhidi ya Stoke City, Liverpool na Wigan na italazimika kushinda mechi zote ili kujihakikishia ubingwa.

Kwa upande wake, Manchester United imebakiza mechi tatu dhidi ya Tottenham, Sunderland na Stoke City.

source nifahamishe