Monday, May 10, 2010

Chelsea Ndio Mabingwa wa Uingereza


Wazee wa darajani Chelsea wamekatisha matumaini ya Manchester United kutwaa ubingwa wa Uingereza kwa mara ya nne mfululizo baada ya kuunyakua ubingwa wa Uingereza kwa kutoa kipigo cha nguvu kwa Wigan kwa kuiburuza magoli 8-0.
Magoli manane waliyobugizwa Wigan Athletic leo kwenye uwanja wa Stamford Bridge yameiwezesha timu ya Chelsea kutwaa tena kombe la ubingwa wa ligi ya Uingereza kwa mara ya nne katika historia ya timu hiyo.

Ushindi wa magoli 4-0 ilioupata Manchester United dhidi ya Stoke City haukuweza kuwasaidia kunyakua taji la ligi ya Uingereza kwa mara ya 19.

Magoli matatu ya Didier Drogba kwenye kipindi cha pili yalimwezesha kuwa mfungaji bora wa ligi ya Uingereza kwa msimu wa mwaka 2009/2010.

Magoli mengine ya Chelsea katika ushindi wa leo yalifungwa na Nicolas Anelka, Salomon Kalou, Ashley Cole na Frank Lampard.

Kocha wa Chelsea amekuwa miongoni mwa makocha wachache sana katika ligi ya Uingereza ambao walifanikiwa kutwaa ubingwa katika mwaka wao wa kwanza wa kuanza kazi.

Chelsea sasa ina mpango wa kuongeza kombe jingine kwenye hazina yake mwaka huu wakati itakapopimana ubavu na Portsmouth kwenye mechi ya fainali ya kombe la FA itakayochezwa jumamosi ijayo kwenye uwanja wa Wembley.


source nifahamishe

No comments:

Post a Comment